Saturday, August 17, 2013

MADRASATUL NNAJJAR ISLAMIYAH - MWANANYAMALA KWA KOPA

MADRASATUL Nnajjary Islamiya ipo nyumbani kwa mlezi wa madrasa hiyo Mzee Abbasi Hamza Masoud, Mwananyamala kwa Kopa Jijini Dar es Salaam.  

Madrasa hii ni maarufu kwa wakazi wa maeneo hayo kutokana na kazi nzuri inayofanywa na walimu ya kuwafundisha wanafunzi wa Kiislamu dini yao. 
Madrasa hii ilianzishwa na mlezi huyo wa madrasa Abbasi Hamza Masoud mnamo mwaka 1963 ikiwa na wanafunzi wasiopungua 15, wasichana kwa wavulana. Kwa kipindi hicho Ustaadh Abbas alifanya kazi kubwa sana ambapo wanafunzi walikuwa wakiongezeka siku hadi siku.  

Mpaka hivi sasa wapo wanafunzi 125 wasichana kwa wavulana, masomo yanayotolewa madrasani hapo ni Fiqh, Tawheed, Sira, Hadithi, Tafsiri ya Qur’an, Hifadhi ya Qur’an na Qur’an kwa njia ya Tajwidi.  

Kwa sasa madrasa hii ipo chini ya usimamizi wa Ustaadh Ahmad Issa, Zuberi Issa, Khalid Abbas na Zuberi Ramadhani. 
Upo utaratibu ambao umewekwa na walimu kwa kila mzazi kulipa Pesa Maalum kwa kila baada ya mwezi ili kuweza kuwasaidia walimu pesa za matumizi yao binafsi.  

Hata hivyo walimu hao wamesema wazazi wa wanafunzi wamekuwa wagumu kutoa pesa hizo bila ya kujali kwamba nao wanahitaji kuishi na kujikimu katika mambo mbalimbali.  

Madrasa Nnajjary inakabiliwa na tatizo kubwa la ukosefu wa vifaa vya kufundishia pamoja na vikalio kama vile mikeka, majamvi na hata magunia na pia hulazimika walimu pamoja na wanafunzi kukaa sehemu ambayo haina mikeka.  

Madrasa hii ina sehemu yake ya kujitegemea na ipo katika mikakati ya kukifanyia chuo ukarabati wa kutosha kwa sababu hakipo katika hali ya kimadrasa. 
Hivyo, wito umetolewa kwa Waislamu wote wajitokeze kwa wingi kutoa sadaka zao za hali na mali ili kufanikisha mikakati hiyo. 

No comments:

Post a Comment