Siku
ya Ijumaa ni siku bora na tukufu miongoni mwa
siku za dunia, Mtume (S.A.W)Rehma za M/Mungu zimshukie Juu yake na Amani ameitaja siku ya Ijumaa kama hivi :
“Bora ya siku uliyochomozewa na jua ni siku ya
Ijumaa, ndani yake Ameumbwa Adamu ndani yake ametiwa peponi. Na ni
ndani yake (siku hiyo) alitolewa humo (peponi)
na wala hakitasimama kiyama ila ndani ya siku ya
Ijumaa”. Kama alivyosema Mtume hadithi imepokewa na Imamu
Muslim.
Zimepokelewa
hadithi nyingi kutoka kwa Bwana Mtume (S.A.W)Rehma za M/Mungu zimshukie Juu yake na Amani zikitaja
fadhila na ubora wa siku hii ya Ijumaa. Hii ni
siku ambayo umo ndani yake wakati (muda fulani)
ambao mja hamuombi Mola wake ndani yake chochote cha kheri ila humpa.
Ni kwa ajili ya
fadhila hizi tulizozitaja na nyinginezo, Allah
akaichagua siku hii kuwa ni Idi (sikukuu) ya
kila juma (wiki) ya waislamu.
Akawaamrisha waja
wake kuipa umuhimu wa pekee siku hii, wajipambe
kama walivyoelekezwa na kufundishwa na Mtume
wao.
Waache shughuli zao na waharakie kuiendea
ibada ya swala ya Ijumaa. Wakutanike pamoja
ndani ya siku hii ili iwe ni nembo, alama na
kielelezo cha umoja wao na dalili na ishara ya
nguvu yao. Siku hii ni zawadi kwa Umma wa Nabii Muhammad (S.A.W)Rehma za M/Mungu zimshukie Juu yake na Amani
kwani ni sababu ya kufutiwa dhambi zao na ni
kirudufisho cha ujira na thawabu.
Lakini
kwa masikitiko makubwa, uzoefu unaonyesha kuwa
waislamu wamekuwa ni watu wa kuzembea na kupuuza
kila kitu. Hata kufikia kiasi cha kudharau
matukufu ya dini yao yaliyotukuzwa na Mola
Muumba wao, huu ni msiba mkuu na haya ni
maangamivu. Leo siku ya Ijumaa machoni na
mioyoni mwa waislamu wengi si cho chote na wala
si lo lote ila ni siku tu kama zilivyo baki ya
siku nyingine za juma. Hili halihitaji ushahidi
kwani linashuhudiwa bayana na kila mmoja wetu.
Waislamu tumeipuuza siku yetu tukufu ya Ijumaa,
siku iliyokuwa na nafasi,cheo, daraja na
iliyopewa umuhimu wa pekee na mababu zetu
(wahenga). Wazee wetu hao wema waliutambua
umuhimu, utukufu na ubora wa siku ya Ijumaa,
hivyo wakawa wakiingojea kwa hamu na shauku kuu.
Waliingojea kama mtu mwenye kiu ayangojeavyo
maji baridi au mithili ya mgonjwa aingojeavyo
siku ya kupona na kupoa kwake. Wakawa wanakoga,
wananadhifisha nguo zao, wakajitia manukato na
wakienda mapema msikitini kuhudhuria swala ya
Ijumaa. Wakienda msikitini ilhali wamefunikwa na
staha, heshima, utulivu na unyenyekevu. Nyoyo
zao zikiwa zimesheheni khofu ya Allah Bwana
Mlezi wao na ndimi zao zikiwa majimaji kwa utajo
(dhikri) wa Mola wao. Macho yao yakiwa
yamesitiriwa na maharamisho ya Allah, hata
wakiingia msikitini kila mmoja wao akiwania
kuchukua nafasi iliyo karibu na khatibu; nafasi
ya mbele. Walifanya hivi kutokana na kupupia
kwao kuhodhi fadhila za safu ya kwanza na
kustafidi na khutba. Khatibu anapopanda juu ya
mimbari na kuanza kukhutubu, huwa makini, nyoyo
zao zikizingatia, usikivu (masikio) wao huwa
wazi. Khatibu hamalizi khutba yake ila huwaliza
wote; janibu ya twaa na janibu ya maasi. Janibu
ya maasi hulia kutokana na kuichelea adhabu na
ghadhabu ya Allah. Wakati ile janibu ya twaa
ikilia kutokana na tamaa ya fadhila na thawabu
za Allah.
Enyi
ndugu waislamu, tuchungeni adabu za siku hii
tukufu, tujinadhifisheni, tujipambeni na
tujitieni manukato kwa ajili ya siku hii adhimu.
Tutokeni majumbani mwetu kwa unyenyekevu
kuelekea kwenye nyumba za Allah. Twendeni mapema
na tukiingia msikitini kila mmoja wetu akae kwa
adabu, heshima, staha na utulivu. Tutahadharini
na kufanya kitendo au kusema kauli itakayomuudhi
Allah, Mtume wake na waja wake mithili ya
kukata/kukengeuka shingo za watu. Tueleweni
kwamba kuwaudhi waislamu ni jambo linalopomosha
ujira na kubatilisha thawabu adhimu za Ijumaa.
Atakayeingia msikitini miongoni mwetu na ilhali
khatibu anakhutubu, basi na asikae chini ila
baada ya kuswali rakaa mbili khafifu (nyepesi).
Tunapomaliza kuitekeleza fardhi hii ya swala ya
Ijumaa, tusiwe na haraka ya kutoka msikitini.
Tukae tuswali suna, tulete dua na tumuombe Mola
wetu maghfira, radhi na uongofu. Mola wetu
Mtukufu tunamuomba airejeshe haiba na utukufu wa
siku ya Ijumaa katika nafsi, nyoyo, roho na
miili yetu Amiin.
Tunawatakia Ijumaa Njema.
Tunawatakia Ijumaa Njema.
No comments:
Post a Comment