Wednesday, July 31, 2013

WASIFU WA HABIB AHMAD BIN ABUBAKAR BIN SUMAYT, radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie


Shaykh Abdallah bin Muhammad bin Swaleh Baakathir (radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie), mmoja kati ya wanazuoni wakubwa wa zama zake alirushwa roho na jambo moja akiogopa sana kwamba watu wasifike hadi ya kutotambua neema kubwa waliyokuwa nayo. Akiogopa kwamba wakiacha kuitambua neema hiyo, hapatakuwa tena na shukurani na shukura ni kufuli ya neema. Ikifanywa shukura, neema hubakia. Zaidi kuliko hayo ni kwamba neema ile hustawi ikaingia na baraka. Na huvuta neema nyingine ambazo mtu kamwe hazikumpata kumjia katika mawazo yake. Kwani si anasema Azza-wa-Jaala, "lau matashukuru hakika hakika nitakuzidishieni”. Aya haifafanui kitakacho zidishwa ni kipi na wala kitazidishwa kwa kiwango gani. Na madamu hayo yanasemwa na Mola ambaye yeye mwenyewe kajiita Shaakhir, mwingi wa kushukuru, basi mawazo ni huria. Shaykh Abdallah Baakathir (radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie) anataja dukuduku lake mwanzo wa kitabu chake cha al-Ashwaaq anasema hivi, “kupatikana mtukufu huyu na watu mithali yake katika zama hizi ni neema kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Anaitambua mwenye kuitambua na mjinga nayo, yule ambaye ni mjinga nayo. Tunamwomba Yeye taala atupe sisi tawfiqi ya kusimama na kushukuru neema zake zote zile za nje na ndani.
Na anaendelea kusema, “au wanazijua lakini wanazikataa na hawazishukuru.” Hapa Shaykh Abdallah anaashiria kuwa neema huwapo na mtu akaikataa.
Al-habib Ahmad bin Abubakar bin SumeitJe, neema hiyo anayoizungumzia Shaykh Abdallah Baakathir ni neema ipi? Hiyo ni neema ambayo pengine leo watu wa Unguja na Afrika Mashariki nzima wameisahau, nayo ni kuwepo kwa Al-Habib Ahmad bin Abi-Bakar bin Sumayt (radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie) miongoni mwao.  Neema ambayo al-Habib Ahmad bin Umar bin Sumeyt (radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie) alikwisha bashiria kuzaliwa kiasi miaka ishirini kabla ya ujudi wake. Na Leo ni Miaka thamanini na sita toka kutawafu kwake.
Shaykh Abdallah Baakathir anamweleze hivi basi, Shekhe wake, al-Habib Ahmad bin Abi-Bakar bin Sumayt mwanzo mwanzo wa kitabu chake cha al-Ashwaqq, "Bwana mwenye sharafa kuu na utukufu mkuu, aliyekunywa kifu yake ilmu zote zile za akili na kupokea, mwenye kukusanya fani za lugha fasaha, mtatuaji wa mishkeli na mtanzuaji wa mitata. Nadra wa zama na pambo la miji na Mufti wa pekee aliyekusanya ya fadhila na matukufu.... nilisoma kwake vitabu kadhaa wa kadhaa na huyu ni Bwana ambaye mazoe yake ni kutembea kwenye bustani za ilmu na ma’arifi na kuchuma hikma na zile ilmu zenye kufichika baina wino na ibara. Aliyepweke katika kuhakiki masaaili na mpweke wa zama zake katika kudiriki undani wake. Kawaswahibu ma-Qutbu na Mashekhe wakubwa wa zama zake, na mawalii ma-‘Arfina, wanazuoni wahakiki wa dahari yake. Na kwao kapata enga enga na malezi na madadi. Na  wao wakamshuhudia kwa matukufu walionayo na ukamilifu wake. Wakamhisabu kuwa yeye ni mmoja wapo ya rijali waliokamilia na wakamfungulia mapazia kumjulisha siri za tarika na hakika zilizomo humo. Na wakamnywesha kinywaji safi cha ilmu ladunniya. Kutokana na baraka zao Mwenyezi Mungu kadhihirisha mangapi kwenye ulimi wake na kalamu yake, yale ambayo yamefichika kwenye fahamu za wengine, na akamimina kwenye maji ya matamko yake matamu yale ambayo yanakonga kiu cha figo cha wanazuoni wa wanazuoni. Ana shuhudiwa kwamba katika ilmu za hakika na maarifi yeye ni Imamu na mzuri aliyoje kuwa Imam. Na kwamba yeye ni nguzo marji'i ya watengwa makhsusi na watu wa kawaida kwenye fani zote za lugha na pia sharia na hukumu.....”
Zaidi ya Shaykh Abdallah Baakathir, Habib Ahmad bin Sumayt alikuwa pia ni Shekhe wa Al-Habib Umar bin Ahmad bin Sumayt, Habib Abdulrahman bin Ubaydillah, Shaykh Sulaiman Alawy, Shaykh Hassan bin Amer na Shaykh Burhan Mkele, kuwataja kwa uchache. Wanazuoni wa zama, ambao matukufu yao hayahitaji kupigiwa debe.
                                     KWA MAKALA NYINGI ZAIDI TEMBELEA