Thursday, August 01, 2013

WASIFU AL-HABIB SAYYID UMAR ABDALLAH BIN SHAYKH ABI-BAKAR BIN SALIM (MWINYI BARAKA), radhi za Mwenyezi Mungu zimshukie

Bismillahi twanza kwa jina la Mola Rahman, aliye Rahim. Mwingi wa rehema na mkarimu, mwenye hazina isiyoisha asilani, Ar-Razzaq.
Mwinyi Baraka peter sanders photosAl-Habib As-Sayyid Umar Abdallah bin Abi-Bakar bin Salim ama kwa umaarufu wake Mwinyi Baraka (radhi za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na wazee wake), shekhe wa mashekhe zetu na ruwaza ya nyoyo zetu, ni kioo cha ilmu na tarika kwa watu wa Afrika Mashariki.
Al-Habib Umar Abdallah ndiye aliyemjazi Shaykh wetu kipenzi as-Shaykh Al-Faqeer Ahmad bin Muhammad bin Shaykh Msiha (radhi za Mwenyezi MUngu zimwalie) tarika Qadiriyyah na tarika ya mabwana wetu watukufu wa Hadhramut wa Ba'Alawi.
Katika kurasa hii tutaandika kwa ufupi juu ya mtukufu wetu huyu aliyezaliwa huko Zanzibar mwaka 1917 na kufishwa huko Ngazija (Commoros) mwaka 1988, ambapo ndio ilipo rawdha yake tukufu. Nasabu yake al-Habib Umar inarudi kwa Bwana wa viumbe  na wana wa Adamu, sala za Mwenyezi Mungu na salamu zake zimshukie na Aali zake na Sahabaze. Kwa upande wa baba yake nasabu yake inapita kwa Sayyidina Abi-Bakar bin Salim na upande wa mama ni Jamali-Llayl.
Al-Habib Sayyid Umar Abdallah, alibobea katika ilmu zote mbili, yaani ilmu ya dini na ilmu ya skuli. Allianza kusoma ilmu ya dini angali mdogo kutoka kwa Ami yake Sayyid Abdul-Fattaah bin Ahmad Jamali-Llayl (maarufu Shariffu Abudu, radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie) ambaye ndiye aliyekuwa mlezi wake baada ya kufiliwa na wazee wake. Sayyid Abdul-Fattaah pia ndiye aliyekuwa wa kwanza kumwingiza Habib Umar katika tarika Qadiriyyah kama alivyobainisha kwenye ijaza aliyowajazia muridi wa al-Majalis el-Ulaa.
Mwaka 1940, Mwinyi Baraka alijiunga na Makerere University kusoma ilmu ya juu na mwaka 1951 alijiunga na School of Oriental and African Studies (SOAS), London ambapo alisoma Arabic na Islamic Law. kati ya walimu wake wakiwemo M.Cowan na J.N.D. Anderson. Mwaka 1961 Habib Umar Abdallah alijiunga na Oriel College, Oxford na kuchukua BA in Islamic Studies. Katika thesis yake Al-Habib aliandika juu ya falsafa ya kiisilamu, angalia kitabu cha Felicity ambacho kimetolewa na Majaalis Qadiriyyah Mwinyibaraka Uwesiya.
Habib Umar Abdallah alisoma kwa mashekhe wengi waliobobea katika ilmu mbali mbali huko Unguja na Shaykh wake mkuu kabisa alikuwa Al-Habib As-Sayyid Umar bin Ahmad bin Abubakar bin Sumayt (radhi za Mwenyezi Mungu ziwaalie wote), mwanazuoni wa wanazuoni na shekhe wa mashekhe zetu. Alimlazimu pia Shaykh Sulayman bin Alawy, mwanazuoni mkubwa kabisa aliyekuwa na mapenzi makubwa kwa bwana Mtume na Aalil-Bayt, sala na salamu za Mwenyezi zimshukie Bwana wetu na watu wa nyumba yake. Shaykh Sulayman al-Alawy (radhi za Mwenyezi Mungu zimshukie) ndiye aliyeshika nafasi ya Al-Habib Umar bin Sumeyt, Al-Habib alipoihama Unguja na kurejea Ngazija, rawdha yake bwana huyu mtukufu ipo huko Ngazija na kila mwaka hufanywa hawl kubwa huko na wapenzi wake kukusanyika kwa wingi toka kila pembe ya dunia, Mwenyezi Mungu atunufaishe nae. Mengi juu ya matukufu ya mabwana hawa wawili, yaani Al-Habib Umar na Shaykh Sulayman (radhi za Mwenyezi Mungu ziwaalie) yamo mbioni kuchapwa na mmoja wa mashekhe zetu, na Mwenye Enzi amjaliye kuyafanikisha hayo.
Habib Umar Abdallah alikuwa ni mwingi wa safari na kila alipokwenda ulimwenguni hakuacha kufanya Da'awa na kutafuta wanazuoni wa miji hiyo na kuchukua ilmu kutoka kwao. Miongoni mwa wanazuoni aliochukua ilmu kutoka kwao ni Sayyid Abdul-Rahman bin Ubaydillah wa Hadhramut, Sayyid Alawi al-Maliki wa Makka, Sayyid Alawi al-Haddad wa Malaysia na wengineo wengi.
Habib Umar Abdallah amepokea ijaza ya tarika Qadiriyya kutoka kwa mashekhe tofauti wa nchi mbali mbali. Miongoni mwa mashekhe waliompa ijaza na u-Khalifa wa Tarika hii tukufu ni mjukuu wa Sayyidina Abdulkadir Jailani (Qudusu Sirru), Sayyid Tahir Allaudin (radhi za Mwenyezi Mungu zimshukie) aliyekuwa msamizi wa rawdha ya Al-Gawth Azzam huko Baghdad kabla ya kuhamia katika nchi ya Pakistan. Zaidi kuhusu Sayyid Tahir angalia tovoti ya wanafunzi wake, www.yamurshid.com
Hapa tumedondoa kwa uchache kuhusu Habib Umar Abdallah Mwinyi Baraka, kwa undani zaidi wa maisha yake na matukufu yake, haya Insh-Allah kwa idhini yake Subuhanna-wa-Taala yamo mbioni kuandikwa katika kijitabu na mmoja wa mashekhe zetu. Basi tuwe na subira na Mola amjalie mwandishi uwezo na nguvu na uhai na afiya kuyaandika hayo ya Habib wetu nasi Insh-Allah tupate kuelimika kwa hayo. Labda kwa kufungia haya machache tunukulu maneno ya Imam wa Makka wa wakati wake, Shaykh Bin Baaz. Katika kijtabu kilicokusanywa na al-Habib al-Faqeer Shaykh Ahmad juu ya safari za al-Habib ulimwenguni, kiitwacho Mwinyi Baraka katika Ulimwengu wa Uislamu, al-Faqeer Shaykh Ahmad ananukulu maneno haya:
Akielezea mwenyewe Al-habib kuwa kila alipokua Makka iliyonawirika, al-Marhumm Bin Bazz alikuwa akimtanguliza… “Umar swalisha”.  Akimwambia: “Bwana Mtume sala za Mwenyezi Mungu na salamu zimshukie, akisema, Ahli-shsharafaa laa  Ahli-sharaf watu wa Sharaf hupitana kwa Sharaf. Walaa Yaa arifa Ahli sh-sharaf, wala hawawajui watu wa Sharaf, Illa Dhawish Sharaf, ila ambao ni watu wa Sharaf”. Kijitabu kilichotajwa hapo juu kinapatikana katika tovoti ya www.al-faqeer.com
Maneno hayo ni kweupe kabisa na wala hayahitaji kuyaeleza wa urefu. Huyo ndio al-Habib Umar Abdallah bin Shaykh Abi-Bakar bin Salim (radhi za Mweneyi Mungu zimshukie).

                                    KWA MAKALA NYINGI ZAIDI TEMBELEA