Thursday, August 01, 2013

Wasifu wa SHAYKH SULAYMAN BIN MUHAMMAD AL-ALAWIY, radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie.

Wasifu wa SHAYKH SULAYMAN BIN MUHAMMAD AL-ALAWIY, radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie.
Sheikh Suleiman Al-alawyKatika miaka sitini iliyopita Msikiti Gofu ulipata hadhi kwa Shaykh Sulayman bin Muhammad al-Alawiy, radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie. Hapa, natufuate basi ule muongozo wa; mwite mwanachuoni mkubwa akupe wasifu wa mwanachuoni mkubwa mwenzake. Na kwa mintarafu hii wa kusema juu ya Shaykh Sulayman bin Muhammad al-Alawiy na awe al-Habib Abdulkadir bin Abdulrahman bin Umar al-Junayd, radhi za Mwenyezi Mungu zimwalie, maarufu kwa jina la Sharif Junayd mjini Dar-es-salaam na kwengineko Tanzania. Na yeye kwenye chuo chake cha al-‘Uquudu Al-Jaahizah. Kwa hakika Sharif Junayd kamtia Shaykh Sulayman bin Muhammad bin Sulayman bin Said al-Alawiy (pichani kushoto) katika kundi la mashekhe zake. Hiyo ni fahari juu ya fahari kwani machoni mwa wanachuoni wa wanachuoni Sharif Junayd ni mwanachuoni. Katika hali kama hii kauli yake Sharif Junayd hiyo ingalitosha lakini dharura za wakati na uchache wa mizani ulionea katika zama zaetu unatulazimisha tuenedelea mbele zaidi kuliko hivyo.
sharif junaydBasi tunanukulu maneno ya Sharif Junayd (pichani kulia) juu ya Bwana huyo, “alikuwa mwanazuoni aliyepea katika uwanazuoni na bahari ya ilmu iliyojaa ilmu tamu tamu na safi, ambaye kafika kwenye kilele cha pekee kwenye ilimu na hasa ilimu za lugha kama vile nahuu na sarfu na balagha na mantik... Na licha ya kuwa katabahhar (kazama katika bahari) ya ilmu mbalimbali alikuwa na istikama. Kaandamanisha ilmu kwa amali hata akafikia utukufu upeo wa matarajio. Alikuwa na khuluka ya daraja ya juu na tawadhu’i iliyofika mbali, alikuwa na moyo wenye kubeba mazito na subira na uvumilivu uliofikia upeo. Alifanyiwa uadui na kwa makusudi aliudhiwa. Lakini kamwe hakudhihirisha ghadhabu. Aliishi maisha ya kukinai na zuhdi na taqwa. (Na akapitisha maisha yake yote kulea muridi kwenye taasisi ya ilmu huko Unguja na huko Msikiti Gofu (karibu na nyumbani kwake)....
Alipofariki Shaykh Suleimani, Sharif Junayd alimlilia hivi, “akili yangu amkani nahisi zimenipotea. Kwa mazito malemevu nimo kwenye ulimwengu mwengine. Si bida’a ikiwa nimezisahau hisi zangu, nikawa wote nimekufa ganzi. Kwani masiku yamenielemea kwa mambo mazito, kwa msiba ulionivunjavunja nisibaki kitu. Kwa kuondoka Ustadh wetu Suleimani, taa ya ilmu na hazina ya ‘irfaani. Bahari ya ilmu, mwenye kuiendea huchota johari atakazo na dhahabu pia. Jamali ya zama, mwema wa utajo. Hatajwi kwa baya tangu ujana wake. Mwingi wa kurejea kwa Mola wake, mcha Mungu mwingi wa kurukuu mwingi wa kusujudu, mwenye kuhuisha ashari kwa Qurani. Zagao za amali zake njema ziwazi na zenye kuonekana. Ni shani kubwa ilioje, yiyo ikiwa ya nuru. Sifa ngapi zenye kuhimidiwa na magapi matukufu ya kumtenga alikuwa nazo, na ambazo maneno yangu hayafiki. Wara’a fika na khuluka zenye kuridhisha na uthabiti ambao kamwe wa pili hana, na haiba na murua na vumilia ya maudhi na khashya ya rahmani. Kalelewa Unguja kwenye mabustani ya ilmu anachuma matunda yenye wingi wa utamu, kapokea kwa wakuu ma-Bwana niwasifu vipi wanazuoni hao rabbani. Mtaje shihabu wetu khasaa mwana wa Sumeyti, mwana kwea wa juu kweye mbingu za ilmu. Wakammiminia siri zao na kwazo akawazidi kimo wote wa rika yake, ai moyo wangu na huzuni zangu leo kaniondokea. Hayuko tena kwenye duru wala kwenye majengo, ai moyo wangu na simanzi zangu. Kwani ye' ni mwezi wa mwisho kuduru kwenye midani, sasa kumekuwa kiza tangu kuuka kwake na totoro imetawala. Ewe ni kuu huzuni zangu na mkubwa mno msiba wangu, furifuri machozi yangu furifuri yanamiminika. Nikiuambia moyo subiri, huniambia subira si uwezo wangu.... Ewe baba wa Zamil ghafula umeondoka na kughibu, ewe pweke wa zamani umeghibu hali ya kuwa sisi kubwa haja yetu kwako, katika kila shani.... Na vikulilie vitivo vya ilmu. Na vilie vururu visiwe na kizuizi. Ikulilie Unguja kwani buruji ya ilmu nguzoze zimedamirika. Naapa machozi na kilio changu yatadumu urefu wa zama. Kaburilo likiwa ardhini ewe mkuu wa matukufu basi lilo liko kwenye pepo ya Jinani.... furahika basi kwani milele utabaki utajo wako mwema na huo ni umri wa pili. Lala usingizi macho tele kwenye bustani ya kaburi, hali umefurahika kwa Raufu na Rayhani.... Ewe Rabbi huyu mja Wako, mgeni Wako, hela mpokee kwenye dari ya ridhaa na nyumba ya amani. Na mwonjeshe kwa fadhila Zako maji ya ridhaa na afua Yako, na mkuruba na maghfira Yako. Na tupe ujira Ewe Rabbi na tupe badili miongoni mwetu, na tupe kheri na ihnsani. Na juu ya kaburi lake yaanguke mawingu ya radhi, na yawe ya kudumu urefu wa zamani."
Wasifu huu wa Shaykh Sulayman al-Alawiy umetoka katika kitabu juu ya maisha ya al-Habib al-Imam Ahmad bin Hassan al-Attas, radhi za Mwenyezi Mungu ziwaalie wote wawili, kitabu kilicho njiani kuchapwa.